McEddy Elroy

Friday, November 24, 2017

Wabunge wa Kenya waketia viti vipya



Viti vipya vya bunge
Bunge la Kenya lililokarabatiwa na ambalo limekuwa gumzo kubwa kwa sababu ya gharama ya viti vya bunge hilo, hatimaye limefunguliwa rasmi na rais wa nchi hiyo Mwai Kibaki.
Viti hivyo vimegharimu dola 3,000 za kimarekani kwa kila kiti kimoja vikiwa jumla ya 350 vimetengenezwa na kitengo cha magereza nchini humo.
Zabuni ya kwanza ya kutengeneza viti hivyo ilitolewa kwa kampuni moja ya nje lakini ilifutwa baada ya baadhi ya wabunge kugundua kila kiti kingegharimu dola 5000 za kimarekani.
Maafisa wanasema ukarabati huo uliogharimu dola milioni 12 utaliweka bunge katika mfumo mpya wa kisasa wa komputa.
"Mabadiliko tunayoyafanya yataleta mabadiliko chanya katika uongozi," spika wa bunge Kenneth Marende ameiambia BBC.
Amesema mfumo wa kupiga kura wa elektroniki utawawezesha wabunge kupiga kura kwa uhuru wao binafsi kuliko kulazimika kupiga kura kwa kuhofia vyama vyao.
"sasa mbunge atakuwa peke yake, huru kabisa binafsi, atafanya maamuzi yake na kubonyeza tu kitufe."
Mwandishi wa BBC Odeo Sirari mjini Nairobi, anasema baadhi wanaona viti hivyo kuwa ni vya gharama kubwa sana kuliko mabunge mengine katika jumuiya ya madola.
Waziri mkuu wa Kenya Raila Odinga na rais Mwai Kibaki pamoja na wabunge ni miongoni mwa wanaolipwa mshahara wa juu sana barani Africa.
Wabunge walifurika katika jengo hilo lililokarabatiwa wakati rais na spika wakiongoza utaratibu wa sherehe za ufunguzi.
Ukarabati huo ulianza mwezi Aprili mwaka 2010 na ulikuwa umepangwa kuchukua mwaka mmoja kumalizika lakini ulichelewa kwasababu ya utata ulioghubika zabuni yake, mwandishi wetu anasema.
Bunge la zamani
Mbunge John Mbadi, katika kamati ya uwekezaji aliongoza upinzani juu ya zabuni ya kwanza.
"hatukuweza kuelewa ni kwa vipi wabunge wangekuwa wanakaa katika viti vinavyogharimu karibu shilingi 400,000 za Kenya kama dola 5,000, ambazo kwa kiwango chochote cha kawaida zingeweza kujenga nyumba kwa wananchi kadhaa," ameiambia BBC.
"ilikuwa ni upuuzi," amesema.
Mwandishi wetu anasema watu wengi wamelalamika kuwa gharama za sasa bado ni juu.
David Langat, anayesimamia uzalishaji katika magereza nchini Kenya, amesema vifaa vyote vilivyotumika vilitoka nchini Kenya lakini gharama za viti zimekuwa kubwa sana.
Ameiambia BBC kuwa viti hivyo vyenye uzito wa kilo 50 kila kimoja vina kinga dhidi ya moto na vina dhamana ya miaka 30.
Kwa sasa Kenya ina jumla ya wabunge 220 lakini ukumbi huo umewekwa viti 350 idadi ambayo watachaguliwa katika uchaguzi ujao mwezi Machi kwa mujibu wa katiba mpya.