McEddy Elroy

Thursday, June 24, 2010

VURUGU ZA WAGOMBEA JIMBO LA KALENGA

Na Mwandishi wetu,Iringa

Juni 26: SIKU chache tu baada ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,Abbas Kandoro kadiwa kuvunja sheria mpya ya kudhibiti matumizi ya fedha kwenye chaguzi, Mkurugenzi Chuo cha Benki Kuu (BoT), kanda ya Mwanza,Dk.William Mgimwa na Mkurugenzi Msaidizi wa umwagiliaji Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika,Mhandisi Gabriel Kalinga pia wanadaiwa kuvunja sheria hiyo.

Kama ilivyo kwa Kandoro, Dk.Mgimwa na Mhandisi Kalinga pia wanawania jimbo la Kalenga lililopo Iringa vijijini ambalo kwa sasa linashikiliwa na Stephen Galinoma ambaye hata hivyo amekwishatangaza kutogombea tena.

Hivi karibuni, Mkuu huyo wa Mkoa wa Mwanza, amedaiwa kukiuka sheria hiyo kwa kumwaga misaada mbalimbali na kuwalipa fedha watu ambao hukodi pikipiki na kupita nyumba hadi nyumba wakimnadi ili wananchi wampigie kura wakati ukifika.

Aidha, Mtumishi huyo wa BoT-Mwanza na mtumishi wa Wizara ya kilimo,chakula na ushirika wameingia kwenye utata wa sheria hiyo wakidaiwa kuanza kampeni mapema kwa kufanya mambo tofautitofauti.

Wakati Dk.Mgimwa anadaiwa kufanya mikutano na kugawa fedha, kutoa fedha za kadi kwa wanachama wapya wa CCM na kununua kinada cha kwaya katika kanisa katoliki kata ya Maboga, Mhandisi Kalinga anadaiwa kugawa vitenge kwa kina mama wa jimbo hilo.

Hata hivyo, Dk.Mgimwa na Mhandisi Kalinga kwa nayakati tofauti wamekanusha madai hayo huku wote wakidai kuwa ni mbinu chafu za kisiasa zinazovurumishwa na wabaya wao wa kisiasa.

Yapo madai kwamba,Dk.Mgimwa amekuwa akifanya mikutano na viongozi mbalimbali wa CCM na kuwagawia fedha kwa lengo la kuwashawishi wamchague muda ukifika.

Aidha,Dk.Mgimwa anadaiwa kununua kinanda cha kwaya katika kanisa Katholiki la kata ya maboga kwa lengo la kuwashawishi.

Pia anadaiwa kutoa fedha kwa makatibu wa matawi wa CCM za kulipia kadi kwa wanachama wapya wa CCM ili wampige kura kwenye kura za maoni.

Madai hayo yanapata nguvu baada ya Katibu wa uchumi na mipago wa CCM kata ya Maboga, Jordan Kisinini ambaye anadaiwa kuwa ni mfuasi mkubwa wa Mgimwa kukamatwa na kadi tatu akidaiwa kuwa katika zoezi la kugawa kadi nyumba hadi nyumba.

Kwa upande wake, Mhandisi Kalinga anadaiwa kugawa vitenge kwa kina mama wa jimbo la Kalenga kwa lengo la kuwashawi wampigie kura wakati ukifika.

Hata hivyo, Dk.Mgimwa alikiri kuchangia kitu alichokieleza kuwa ni fedha nyingi kuliko waumini wengine katika kanisa Katholiki la Maboga ili kusaidia jitihada za kanisa hilo kununua kinanda na Jenereta ingawa alisema hakutoa fedha zote za kununua kinanda hicho.

“Mimi sikwenda pale (kanisani) kuomba niwafadhili ila walikuwa na ratiba ya kupata Kinanda na Jenereta hivyo wakawa wanatangaza kanisani kila wiki na mimi wakaniletea barua kwa sababu ni kanisa ambalo mimi husali nikiwa nyumbani,…sasa nisichangie kwa sababu nimetangaza kuwania Ubunge?,” alihoji na kuongeza:

“Nilichangia fedha kama waumini wengine walivyofanya labda pengine tatizo linaonekana kwa sababu mimi nilichangia fedha nyingi kuliko waumini wengine”.

Dk.Mgimwa alisema haoni tatizo la kuchangia kanisani na kufanya mambo mengine mazuri kwa jamii kwa sababu hufanya hivyo miaka yote bila kujali anagombea Ubunge au la.

“Mimi nadhani, kuna watu wanafahamu kwamba nikienda Kalenga moto wangu ni mkali ndiyo maana wananiogopa, mbona hawasemi nilivyochagia kwenye Jubilee ya mapadri kule Ifunda,…au kwa sababu na wagombea wenzangu walichangia?, mbona hawahoji kwa nini nasomesha zaidi ya watoto yatima 130 katika shule za sekondari huko Kalenga?,” alihoji.

Aidha, kuhusu fedha za kununua kadi alisema hajawahi kufanya hivyo na kwamba kazi hiyo ni ya CCM.

“Huo ni upuuzi mtupu na huyo Kisinini unayemtaja hata mimi nilisikia tu kwamba kuna mtu anasakamwa sakamwa kwa kukutwa na kadi lakini hicho kitu mimi sikifahamu,” alisema na kuongeza:

“Hata mimi nimesikia kwamba kuna mwanasiasa mmoja ambaye atagombea amewanunua madiwani na wamekuwa wakigawa kadi nyumba hadi nyumba,bado hujalifahamu hilo?”.

Kuhusu kufanya mikutano na kugawa fedha kwa wajumbe,mtumishi huyo wa BoT Mwanza alisema:

“Unafahamu, mama yangu ni mgonjwa kule kijijini (Kalenga), kwa hiyo mara kwa mara huwa nafika kule na kumchukua kumpeleka Dar-Es-Salaam kwa matibabu, sasa ninavyofanya hivyo watu hufikiri nakwenda Kalenga kufanya mikutano ya kampeni”.

Kwa upande wake, Katibu wa Mipango na Uchumi wa CCM kata ya Maboga,Kisinini anayedaiwa kukamatwa na kati tatu akigawa nyumba hadi nyumba, alikanusha madai hayo na kusema taratibu za CCM hazimruhusu kuwa na kadi mpya za Chama hicho.

“Unasikia ndugu yangu, huo ni uongo kupindukia, hakuna ukweli hata chembe,…Kama wanadai kwamba mimi nilikuwa nagawa kadi kwa wananchama ili baadaye wampigie Mgimwa, hebu waulize viongozi wa CCM utaratibu wa kadi ukoje, na kama nilikuwa nazo nilizipata wapi?,” alihoji Kisinini.

Hata hivyo, Katibu wa CCM wilaya ya Iringa vijijini,Luciano Mbossa alithibitisha Kisinini kukamatwa na kadi tatu ambazo hazikuwa zimemfikia kwa kufuata utaratibu wa kadi wa CCM.

Kwa upande wake, Mhandisi Kalinga alikanusha kugawa vitenge kwa wanawake na kusema kwa mara ya mwisho kufika jimboni Kalenga ilikuwa wakati wa siku kuu ya Pasaka.

“Huo ni uongo mtupu, nia ya kuwania ubunge jimbo la Kalenga ninayo lakini sijafanya lolote kwa sababu Chama chetu (CCM) hakijaturuhusu kuanza kampeni”, alisema.

Akizungumzia madai hayo. Katibu wa CCM wilaya ya Iringa vijijini, Mbossa, aliwaonya wagombea kutoingia mgogoro na taratibu za chama pamoja na sheria ya kudhibiti matumizi makubwa ya fedha kwenye chaguzi kwa kuwa kwa kufanya hivyo, wanahatarisha hata nafasi yao ya kugombea.

“Naonya na nasisitiza kwamba yeyote anayekiuka sasa, tusilaumiane mbele ya safari”, alisema Mbossa.



Uteuzi unatarajiwa kuanza mwishoni mwa Julai, mwaka huu, ukitanguliwa na uchukuaji fomu za kuwania nafasi hizo na kwamba mchakato huo utaanza baada ya Bunge la sasa kuvunjwa.

Kwa mara ya kwanza, Uchaguzi Mkuu nchini unatarajiwa kufanyika chini ya uthibiti wa sheria mpya ya Gharama za Uchaguzi iliyotungwa kulenga kuthibiti matumizi ya fedha.

Mwisho


Tuesday, June 22, 2010

FTMT/TMF Iringa Training

Mtaalam na mpiga picha nchini, Mwanzo Millinga (wa kwanza kushoto) akiwaelekeza jambo waandishi wa habari Mkoani Iringa walioshiriki mafunzo ya upigaji picha yalioendeshwa na Flame Tree Media Trust kwa ufadhili wa Tanzania Media Fund.