McEddy Elroy

Saturday, October 1, 2011

Wanyama aina Viboko kwenye moja ya vidimbwi vya mto Ruaha Mkuu vilivyobaki ndani ya hifadhi ya Ruaha

Baadhi ya maeneo katika bonde la Ihefu,ambalo chanzo kikuu cha mto Ruaha Mkuu,yameanza kukauka.

Hali ilivo ndani ya hifadhi

Kadri unavyoelekea Ihefu,mto Ruaha Mkuu unapata uhai

UMWAGILIAJI SAWA,UMEME NAO JE?????????????

Ukichunguza kwa makini,utabaini kwamba uchache wa mvua katika misimu miwili iliyopita siyo chanzo pekee cha kukauka kwa mto Ruaha Mkuu na hatimaye kukauka kwa bwawa la Mtera na mabwawa mengine kama Kidatu na Kihansi.

Kilimo cha umwagiliaji kinachopigiwa upatu mkubwa sana na tamko la Kilimo kwanza, ambacho hufanyika katika maeneo mbalimbali hususani maeneo ya Kapunga huko Mbarali, karibu kabisa na chanzo cha mto Ruaha Mkuu huko katika eneo oevu la Ihefu,kimekuwa ni chanzo kikubwa cha kukauka mto huo.

Kingine ni siasa chafu za baadhi ya wanasiasa wanajali zaidi maslahi yao na kuacha maslahi ya Taifa.Mathalani, Serikali ilikwishatangaza hadi kwenye gazeti la Serikali kwamba eneo flani liihifadhiwe na watu wote waliokuwepo waondoke ili uoto wa asili urejee na hivyo kutiririsha maji mwaka mzima lakini anaibuka mtu mmoja tu tena anayetaka ubunge na kuanza kuwalaghai wananchi kwamba Serikali ilifanya makosa na hivyo wakimchagua yeye atahakikisha wanarejea kwenye eneo hilo,ni nini hiyo kama siyo siasa chafu isiyozingatia maslahi ya Taifa na kwa hakika siasa kama hiyo inaweza kulitumbukiza Taifa katika vurugu na wananchi wake.

Ukiungalia mto Ruaha Mkuu kwa sasa, hauna matumaini kabisa kwa Taifa hili kwa upande wa umeme.Lakini mto huo unaonesha matumaini kidogo kadri unavyoelekea kwenye chanzo chake huko Ihefu.Kumbuka Ihefu ni matokeo ya maamuzi magumu yaliyofanywa na Serikali takribani miaka mitano iliyopita kwa kuwaondoa wafugaji waliokuwa wamevamia eneo hilo.

Kwenye hifadhi ya Ruaha,mto huo umebaki kuwa na hali ya madimbwi madogo madogo ambayo kwa sasa ndiyo uanaokoa wanyama waliomo humo lakini ukiufuatilia hadi Ihefu, utagundua kuwa,kadri unavyoelekea Ihefu, ndivyo unavyokuwa na uhai kidogo kama picha hapo juu, inavyoonesha.

Friday, September 30, 2011

NYATI WAKINYWA MAJI MTO RUAHA MKUBWA,KAMA WALIVYONASWA KUTOKEA ANGANI

MTO RUAHA MKUBWA WABAKI MADIMBWI,HAKUNA MATUMAINI YA UMEME

Maji yanaendelea kuwa bidhaa nadra sana nchini.Hali ya Mto Ruaha Mkubwa (The Great Ruaha) ambao unategemewa sana na mabwawa yanayotumiwa na Shirika la Ugavi wa umeme nchini Tanzania (Tanesco) ya Mtera,Kidatu na Kihansi kuzalisha nishati hiyo, uko katika hali mbaya sana na kwa hakika hakuna matumaini kabisa kama mvua zitachelewa kunyesha.
Blog huu imetenbelea hifadhi ya ruaha wiki iliyopita na kufanikiwa kupata picha mbalimbali za mto huo hapo September 28,mwaka huu, zinaonesha namna hali ilivyo mbaya hali inayotishia ustawi wa hifadhi ya ruaha.
Historia ya hifadhi ya Ruaha haiwezi kutenganishwa na Mto Ruaha Mkuu au Mto Ruaha Mkubwa hivyo bila uwepo wa mto Ruaha Mkubwa, mimea na uoto mwingine wa asili utatoweka vivyo hivyo kwa wanyama ambao ni rasilimali kubwa ya Taifa la Tanzania.
Kwa sasa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha ni kubwa kuliko hifadhi yoyote nchini ikiwa na meta za mraba 20,000 (Elfu ishirini).Ruaha pia ni ya pili kwa ukubwa barani Afrika ikifuata kwa karibu kwa hifadhi ya Salonga iliyoko nchini Jamhuri ya Kidemocrasia ya watu wa Congo.
Tutaendelea kukuletea habari hii kwa kina zaidi. Endelea kuwa nasi.

MTO RUAHA MKUBWA WABAKI MADIMBWI,HAKUNA MATUMAINI YA UMEME

Tuesday, June 7, 2011

MWAKILISHI MSAIDIZI WA THE GUARDIAN IRINGA AFARIKI DUNIA

MFANYAKAZI wa Kampuni ya The Guardian Ltd Mkoani Iringa, Isdory Fungo (41) amefariki dunia.
Fungo alifariki dunia alfajiri ya Juni 07,mwaka huu katika hospitali ya Wilaya ya Makete alikokimbizwa baada ya hali yake kubadilika ghafla.
Taarifa iliyotolewa na Mwakilishi wa Kampuni ya The Guardian Mkoa wa Iringa, Kishede Msuya imesema awali, Fungo alikuwa anaugua malaria na miguu ambapo alipata matibabu Mjini Iringa kabla ya kwenda hospiatli ya Misheni ya Ikonda wilayani Makete kwa matibabu zaidi ambako alilazwa kwa wiki moja na kurejea kwa kaka yake Mjini Makete.
Hata hivyo,akiwa nyumbani kwa kaka yake usiku wa kuamkia jana hali yake ilibadilika ghafla ambapo alikimbizwa katika hospitali ya wilaya ya Makete lakini alifariki dunia muda mfupi baadaye.
Kampuni ya The Guardian inaungana na wafiwa katika msiba huo, ambao marehemu Isdory atazikwa nyumbani kwao Makete.
Kabla ya kuajiriwa na kampuni ya The Guardian mwaka 2008 alikuwa wakala wa magazeti ya kampuni mbalimbali katika kituo cha Makambako wilayani Njombe,kazi ambayo aliifanya kwa zaidi ya miaka 10.
Hadi kifo chake hapo jana,Fungo alikuwa Mwakilishi Msaidizi wa Mkoa wa Iringa wa kampuni ya The Guardian Ltd. Marehemu ameacha mjane na mtoto mmoja.

NIMEREJEA NDUGU ZANGU NAOMBA MNIUNGE MKONO

Wapenzi wasomaji wangu wa blog hii.Naahidi kwamba kwa sasa nimerejea kwa kishindo kukuketea mambo uliyoyakosa kwa muda mrefu.Kwa takribani miezi miwili na nusu nimekuwa sipo sana hewani baada ya computer yangu kuibwa na watu ambao mpaka leo hawajulikani.
Nimejikongoja na nimenunua Computer nyingine na sasa nimerejea tena katika ulingo huu wa upashanaji na uelimishaji jamii yetu.
Twende pamoja.Tanzania yetu sote.

Sunday, March 27, 2011

WATU WANAONIFUATILIA WAIBA LAPTOP YANGU

Habari ndugu wapenzi wa Blog hii muipendayo.
Nasikitika kutoa taarifa kwamba,watu wasiofahamika wameingia ofisini kwangu kwa kutumia Master Keys na kuiba Computer yangu ndogo aina ya Apple na sasa imekuwa ngumu kuwa hewani mara kwa mara kwa sababu ya tatizo hilo.

Hizi huu umenistua sana hususani ikizingatiwa kwamba, wameingia na kuchukua Laptop tu hali inayonipa mashaka kama kweli walikuwa wanatafuta hiyo Laptop au wanatafuta kilichomo kwenye Laptop hiyo.

Pale mezani ilipokuwa Laptop,kulikuiwepo vitu vingi vyenye thamani kubwa kama Mordem ya Internet,Dvcam Camera yenye thamani ya dola za kimarekani 4,000, simu ya mkononi aina ya Nokia ambayo hata hivyo ni mbovu kidogo na ndiyo maana ilikuwa inabaki ofisini,kulikuwa pia na flash mbili moja ya GB mbili na nyingine ya MB 250 na vitu vingine vingi vidogo vidogo ambavyo nina uhakika kama ni vibaka wa kawaida wangevikusanya!.

Nashawishika kuamini kwamba kuna watu walikuwa wananifuatilia hasa baada ya kuwa nimeanza kuichunguza taasisi moja kubwa hapa mkoani Iringa ambayo baadhi ya viongozi na watumishi wake wana tuhuma nzito za ubadhilifu wa fedha za umma.

Nimetoa taarifa Polisi na kupewa RB Na.IR/RB/1666/2011 ya Machi 25,mwaka huu.Naomba dua zenu ili niweze kuipata Computer hiyo na kama kuna watu wananifuatilia, basi wasifanikiwe kunidhuru.

Hata hivyo,nawaahidi wapenzi wangu kwamba pamoja na tatizo hili nitaendelea kuwaletea vitu mlivyozoea hususani taarifa za uchunguzi bila woga wala upendeleo.

Tuko pamoja.!

Thursday, March 10, 2011

POLISI WADAIWA KUJERUHI MWANAFUNZI KWA KIPIGO

JESHI la Polisi mkoani hapa, limetupiwa tuhuma ya kumjeruhi kwa kipigo mwanafunzi wa kidato cha nne wa sekondari ya Efatha iliypo Kitwiru Manispaa ya Iringa wakati wakijaribu kuwatawanya wanafunzi hao Machi 9.

Taarifa za kujeruhiwa kwa mwanafunzi huyo zimetolewa kwa Mbunge wa viti maalum (CCM) Mkoa wa Iringa,Ritha Kabati ambaye alitembela shule hiyo machi 10,mwaka huu kujua tatizo pamoja na kuwa pole wanafunzi.

Mkuu wa shule hiyo,Kenneth Ngelangela alimwambia Mbunge huyo aliyekuwa ameongozana na Meya wa Manispaa ya Iringa,Mstahiki Aman Mwamwindi kuwa mwanafunzi alijeruhiwa kwa kipigo cha polisi ni Giveness Mvamba.

Aidha,Mkurugenzi wa shule hiyo Paul Tabani alisema mwanafunzi huyo alikuwa anauguza majeraha yake nyumbani na kwamba jana walikuwa wanaangalia utaratibu wa kumpeleka hospitali kwa matibabu.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa,Claus Mwasyeba alisema hana taarifa kama kuna mwanafunzi alijeruhiwa na kuomba kama mwanafunzi huyo yupo basi aende ofisini kwake akamwone.

Katika vurugu hizo, alisema hakuna mwanafunzi aliyekamatwa wala kuhojiwa lakini tyaarifa zilizotolewa kwa mbunge huyo zilieleza kuwa baadhi ya wanafunzi hususani wa kike walikamatwa na kutupwa kwenye magari ya polisi kitendo ambacho Mbunge huyo aliunga mkono kwa maelezo kuwa aliwaona wanafunzi hao wakiwa kwenye magari ya polisi kwenye picha za taarifa ya habari ya juzi usiku ya kituo cha ITV.

Vurugu hizo zilizuka juzi asubuhi baada ya wanafunzi hao kuwaweka kiti moto wakaguzi wa shule kanda ya nyanda za juu kusini wakitaka kujua uhalali wa kuzuiwa matokeo ya mitihani ya kidato cha pili, iliyofanyika mwishoni mwa mwaka jana.

Baadhi ya wanafunzi waliozungumza na NIPASHE walisema kuwa, vulumai hiyo ilianza baada ya mmoja wa wakaguzi hao Benadetha Mtitu kuwapa majibu ya hovyo, pale walipotaka kujua sababu za kuzuiwa matokeo ya mitihani yao wakati walitimiza masharti yote ya mitihani hiyo.

“Alituambia ni bora tukalime na wasichana waende kuolewa kwa sababu walikuwa wanapoteza muda bure shuleni hapo kwa kuwa shule hiyo ilikuwa haijatimiza masharti kadhaa,” alidai mwanafunzi wa kidato cha nne,Shamte Mussa wakati akimkariri mkaguzi huyo.

Wanafunzi 500 wa kidato cha pili walifanya mitihani yao baada ya kulipa gharama za mitihani lakini hadi sasa wahawajapatiwa matokeo yao jambo ambalo liliwalazimu kuhoji kama kanuni haziruhusu wanafunzi zaidi ya 80 katika mkondo mmoja kufanya mitihani hiyo kwa nini ofisi ya elimu ilichukua fedha zao na kuwaruhusu wanafunzi wote 500 kufanya mitihani hiyo kisha kuzuia matokeo yao.

Akizungumza shuleni hapo Mbunge Kabati kwanza aliwapa pole wanafunzi hao kwa kuzuiliwa matokeo yao lakini akawataka kuwa watulivu na waendelee kusoma na kwamba yeye binafsi atalifikisha suala hilo kwa Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi.

Kwa upande wake,mkaguzi anayedaiwa kuwatukana wanafunzi hao,Benadetha Mtitu hakupatikana jana lakini Mkuu wa Ukaguzi wa shule Kanda ya Nyanda za juu Kusini,Hebron Mlelwa alikataa kataka kuzungumzia suala hilo kwa madai kuwa limeshafika Wizara ya Eilumu na kwamba yeye si msemaji wa Wizara hiyo.

MWAKALEBELA AIGARAGAZA TAKUKURU MAHAKAMANI KWA MARA YA PILI

MAHAKAMA ya Mkoa wa Iringa,kwa mara nyingine imemwachia huru aliyekuwa mshindi wa kwanza katika kura za maoni nafasi ya ubunge wa Iringa Mjini (CCM),Frederick Mwakalebela (41) na mkewe Selina katika kesi namba nane ya kutoa hongo kwenye mchakato wa kura za maoni iliyokuwa inawakabili.
Mwakalebela pia aliachiwa huru Februari 25,mwka huu na hakimu Festo Lwila wa mahakama ya wilaya ya Iringa kwenye kesi namba 4 iliyokuwa inamkabili peke yake baada ya hakimu huyo kujiridhisha kuwa upande wa mashtaka ulikuwa haujatenda haki kuchanganya makosa mawili kwenye shtaka moja na kusema kuwa upande wa mashtaka ulikuwa na hiari ya kumshtaki tena mahakamani Mwakalebela kama wanaona inafaa kufanya hivyo lakini kwa kutumia kosa moja na sheria moja kati ya mbili walizokuwa wametumia.
Tofauti na kesi namba nne,Mahakama ya Mkoa wa Iringa chini ya hakimu wa mahakama hiyo,Mary Senapee amemwachia huru Mwakalebela na Mkewe Selina baada ya kuridhika na hoja kuu mbili za utetezi uliokuwa unaongozwa na Bsil Mkwatta wa Mkwatta Law Chambers.
Hoja hizo ni kwamba upande wa mashtaka wakati wanapeleka hati ya mashtaka mahakamani ilipindi waonyeshe wazi kwamba Mwakalebela na Mkewe walitoa hongo kwa ajili ya kutaka upendeleo au kupindisha utaratibu wa kawaida kwa niaba ya ofisi yao au mkubwa wao na kwamba waliopokea pia walifanya hivyo kwa niaba ya ofisi zao,biashara zao au mkubwa wao (In relation to his principal affairs or Business).
Kwamba kifungu namba 15(1)(b) cha sheria ya kuzuia na kupammbana na rushwa ya mwaka 2007 kinawahusu watumishi wa serikali au wanaoshikilia ofisi za umma hivyo ni lazima hati ya mashitaka ionyeshe waziwazi maneno hayo.
Hoja ya pili aliyokubaliana nayo ni upande wa mashtaka kutotenda haki kwa kuchanganya makosa mawili kwenye shtaka moja kwa kutumia sheria mbili tofauti – sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa ya mwaka 2007 na sheria ya Gharama za uchaguzi ya mwaka 2010.
Katika hoja ya kwanza Mwendesha mashtaka wa Takukuru Mkoa wa Iringa,Imani Nitume alisema maneno hayo siyo lazima yaonyeshwe kwenye hati ya mashtaka kwani yanaweza kusubiri wakati wa ushahidi.
Hata hivyo,hakimu Senapee alijiridhisha kuwa hoja hizo zina nguvu kisheria na kwamba kuchanganya makosa mawili kwenye shtaka moja si haki pia mahakama haiwezi kusubiri ushahidi ili kujua Mwakalebela na Mkewe pamoja na waliopokea hongo hiyo walikuwa na ´Principals´ wakati wa kutenda kosa hilo hivyo akawachia huru watuhumiwa na kueleza kuwa upande wa mashtaka wanayo haki ya kukata rufaa kama hawajaridhika na hukumu hiyo.
Mwakalebela kwa pamoja na mkewe Selina,wanadaiwa kuwa mnamo mwezi Juni mwaka jana, katika kijiji cha Mkoga Manispaa ya Iringa, walitoa hongo ya Sh.100,000 kwa Mwenyekiti wa kijiji hicho, Hamisi Luhanga ili azigawe kwa wapiga kura 30 wa CCM ili wampigie kura za maoni zilizofanyika Agosti mosi, mwaka jana.

Friday, February 25, 2011

MWAKALEBELA APANGUA KESI YA KWANZA MAHAKAMANI

ALIYEKUWA mshindi wa kwanza katika kura za maoni nafasi ya ubunge wa Iringa Mjini (CCM),Frederick Mwakalebela (41),ameanza kupangua kesi za kutoa hongo kwenye mchakato wa kura za maoni zinazomkabili baada ya kesi ya kwanza dhidi yake, kuondolewa mahakamani.

Aidha, mahakama ya wilaya ilimwachia huru Mwakalebela kwenye kesi namba 4 ya mwaka 2010 iliyokuwa inamkabili lakini hata hivyo, mahakama hiyo haikufuta mashitaka dhidi yake.

Mwakalebela sasa anaelekeza nguvu kwenye kesi namba 8 pia ya mwaka 2010 ambayo inamkabili yeye pamoja na mkewe,Selina, ambayo ipo hatua ya kutolea hukumu pingamizi la kisheria iwapo iondolewa mahakamani au la na kwamba itafikishwa mahakama ya Mkoa wa Iringa,Jumatatu ya Februari 28,mwaka huu.

Hakimu wa mahakama ya wilaya,Festo Lwila aliyekuwa anasikiliza shauri namba 4 dhidi ya Mwakalebela ameondoa kesi hiyo mahakamani na kumwachia huru mtuhumiwa huyo baada ya kuridhika na hoja moja ya upande wa utetezi kwamba kulikuwa na mapungufu ya kisheria kwenye hati ya mashitaka.

Mapungufu hayo ni mtuhumiwa kushitakiwa kwa makosa mawili kwenye hati moja ya mashitaka na hivyo kumfanya mtuhumiwa ashindwe kuelewa kwa usahihi kosa linalomkabili kitu ambacho kinaweza kumfanya ashindwe kuandaa utetezi wake.

Awali,upande wa utetezi ukiongozwa na wakili Basil Mkwata wa Mkwata Law Chambers,uliwasilisha pingamizi la awali la kisheria mahakamani hapo ambalo lilikuwa na hoja tatu.

Hoja hizo ni pamoja na kifungu namba 15 (1) b cha sheria namba 11 ya kuzuia na kupambana na rushwa ya mwaka 2007 alichoshitakiwa nacho mtuhumiwa kilikuwa kinawahusu zaidi watumishi au wanaoshikilia ofisi za umma.

Hoja ya pili ilikuwa kwamba, kifungu Na. 21 (1) ( a) na 24 (8) ya Sheria ya Gharama za Uchaguzi ya mwaka 2010, hakitengenezi kosa kwa sababu vinazungumzia mwenendo usiofaa (unfair Conduct) kwenye kampeni za uchaguzi.

Wakili Mkwata katika hoja yake hiyo alisema katika sheria ya gharama za uchaguzi,hakuna hata sehemu moja iliposema waziwazi kwamba Unfair Conduct ni kosa la jinai na kwamba ni suala ambalo linaweza kutatuliwa nje ya mahakama ikiwemo mtuhumiwa wa Unfair Conduct kuenguliwa kwenye nafasi anayogombea.

Hoja ya tatu ni kwamba hati ya mashitaka haikuandaliwa vyema kwa kugumbukwa na mapungufu ya kisheria hususani kumshitaki mtuhumiwa kwa makosa mawili kwa kutumia sheria mbili tofauti kwenye hati moja ya mashitaka.

Akitoa uamuzi wa pingamizi hilo,hakimu Lwila alizitumpilia mbali hoja ya kwanza na ya pili lakini akakubaliana na upande wa utetezi kwenye hoja ya tatu.

Alisema kitendo cha upande wa mashitaka kumshitaki mtuhumiwa kwa makosa mawili kwenye hati moja ya mashitaka ni kinyume cha sheria kwani mtuhumiwa anaweza asifahamu kwa ufasaha kosa linalomkabili na hivyo kushindwa kuandaa utetezi wake kwa hiyo alimwachia huru Mwakalebela.

“Mshitakiwa anakuwa huru na upande wa mashitaka una hiari, kama bado una-Interest na shauri hili walete upya mahakamani hati nyingine ya mashitaka kwa kuzingatia sheria.
Umati mkubwa uliofurika mahakamani ulionekana kufurahia uamuzi huo na kumfuata Mwakalebela kumpongeza mara baada ya kuteremka kizimbani.

Hata hivyo,Mwakalebela mwenyewe aligoma kuzungumza na waandishi wa habari kwa maelezo kuwa hawezi kuzungumza kwa sababu bado anakabiliwa na kesi nyingine ambayo itarejeshwa mahakama ya Mkoa wa Iringa,Jumatatu ijayo.

Upande wake,Mwendesha mashitaka wa Takukuru Mkoa wa Iringa,Imani Nitume aliwataka wandishi wa habari kuwa na subira na kwamba watajulishwa uamuzi wa Takukuru baada ya hukumu hiyo.
“Jamani haya ni mambo ya kiofisi msubiri tutawaambia hatua tutakazochukua lakini hata hivyo si mmesikia wenyewe,uamuzi wa mahakama ni mzuri na umenyooka,” alisema Nitume.

Mwakalebela alishitakiwa mahamakani hapo kwa madai kuwa, mwezi Juni mwaka huu, katika kijiji cha Mkoga Manispaa ya Iringa alitoa hongo ya Sh.100,000 kwa Mwenyekiti wa kijiji hicho, Hamisi Luhanga ili azigawe kwa wapiga kura 30 wa CCM ili wampigie kura za maoni zilizofanyika Agosti mosi, mwaka huu.

Kuondolewa kwa kesi hiyo mahakamani,inamaanisha kuwa Takukuru wamepata pigo lingine baada ya kesi iliyokuwa inamkabili Waziri wa zamani Joseph Mungai na viongozi wengine wa CCM wawili ya kutoa hongo kwenye mchakato wa kura za maoni pia kuondolewa mahakamani, mwezi Januari,mwaka huu.

Mungai (66) pamoja na Katibu wa Umoja wa vijana wa CCM wa Wilaya ya Mufindi, Fidel Cholela (39) na Moses Masasi walikuwa wanakabiliwa na mashtaka 15 ya rushwa kwenye mchakato wa kura za maoni kinyume na sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa ya mwaka 2007 na sheria ya gharama za uchaguzi ya mwaka 2010 .

Hata hivyo,mwezi uliopita,hakimu Mary Senapee wa mahakama ya Mkoa wa Iringa aliyekuwa anasikiliza shauri la Mungai na wenzake aliliondoa mahakamani shauri hilo baada ya kuridhika na hoja za utetezi lakini akasema Takukuru wako huru kufungua kesi upya kwa kufuata sheria zilizopo.

Alipohojiwa,Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Iringa,Emma Kuhanga alisema kilichofanyika mahakamani si kumfutia mashtaka Mungai na wenzake bali kuondoa kesi mahakamani na kwamba Takukuru wako huru kufungua upya mashtaka.

Alisema tayari wameshapeleka kusudio la kufungua upya mashtaka ambalo lilipelekwa Mahakama Kuu tangu Februari Mosi, mwaka huu.

“Kwa hiyo kinachofanyika hivi sasa ni kupitia hukumu ya mahakama, kupitia upya jalada la kesi ili tufungue upya kesi dhidi ya Mungai na wenzake, tukishafungua tutawapeni taarifa,” alisema Kuhanga.

Monday, February 7, 2011

UPANUZI WA HOSPITALI YA MKOA WA IRINGA WAANZA KUKAMILIKA

Jengo la kujifungulia wajawazito linalojengwa katika hospitali ya Mkoa wa Iringa kwa msaada wa hospitali ya Visenza nchini Italia linavyoonekana hivi karibuni.

AWAMU ya kwanza ya upanuzi wa hospitali ya Mkoa wa Iringa, inatarajiwa kukamilika mwisho mwa mwezi ujao, yaani Machi, mwaka huu.

Upanuzi huo unaogharimiwa na hospitali rafiki na hospitali hiyo kutoka nchini Italia ya Vicenza,unagharimu fedha za kitanzania,Sh.bilioni mbili.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa hospitali ya Mkoa wa Iringa,Dk.Oscar Gabone amesema upanuzi huo unajumuisha ujenzi wa jengo la kujifungulia kina mama litakalokuwa na vitanda 20.

Katika upanuzi huo, limo pia jengo la upasuaji kina mama wajawazito na jengo laghorofa moja la wodi ya watoto litakalokuwa na vitanda 100.

Aidha,licha ujenzi wa majengo, msaada huo pia unajumuisha samani zote za majengo hayo na vifaa vya kisasa vya tiba pamoja na mafunzo ya namna bora ya kuhudumia kina mama na watoto yatakayotolewa kwa wafanyakazi watakaokuwa wanahudumu kwenye majengo hayo.

Hospitali hiyo ya Visenza ya nchini Italia imesaini mkataba na hospitali ya rufaa ya KCMC wa kutoa mafunzo ya namna bora ya kuhudumia kina mama na watoto kwa baadhi ya watumishi wa hospitali ya Mkoa wa Iringa.

Kwa mujibu wa Dk.Gabone,majengo yatakayokamilika Machi 31,mwaka huu, ni jengo la kujifungulia kina mama na jengo la upasuaji kina mama wajawazito hali ambayo itafanya huduma za kina mama wajawazito kuimarika na kuwa bora zaidi hospitalini hapo.

”Nina imani kwamba baada ya upanuzi huu kukamilika huduma katika hospitali yetu (ya Mkoa wa Iringa) hususani kwa kina mama wajawazito na watoto zitakuwa bora sana kwa sababu marafiki zetu wa Italia watatupatia Elimu, Majengo bora, eneo safi la kutolea huduma na vifaa vya kisasa kabisa,” alisema Dk.Gabone.

Saturday, February 5, 2011

UFISADI WATIKISA CHUO KIKUU CHA ELIMU MKWAWA

UONGOZI wa Chuo Kikuu kishiriki cha Elimu Mkwawa (Muce) cha Mkoani Iringa, unakabiliwa na tuhuma nzito za kufanya ufisadi wa aina mbalimbali chuoni hapo.

Ufisadi unaodaiwa kufanywa na baadhi ya viongozi wa chuo hicho ni pamoja na wizi wa fedha za Chuo hicho kupitia mikataba ya wazabuni, upendeleo, kujilipa mishahara mara mbili pamoja na kuendesha akaunti za benki za muda maalum (Fixed Deposit Account) kwa kutumia fedha za serikali au za wafadhili na hivyo kuchelewesha malipo mbalimbali ya watoa huduma na kwa wanafunzi.

Uongozi wa Chuo hicho umethibitisha baadhi ya madai na kuyakanusha vikali mengine huku ukidai kuwa ni njama za baadhi ya watu au wafanyakazi wanaotaka kuchafua taswira ya taasisi hiyo ya elimu ya Juu.

Uchunguzi wa zaidi ya wiki mbili umebaini kuwa kuna wafanyakazi watatu (majina yao tunayo) wa Chuo hicho ambao wamekuwa wakijilipa mishahara mara mbili.

Nyaraka zinaonesha kuwa mfanyakazi mmoja ambaye ngazi ya mshahara wake ni kati ya Sh 318,620/- na 339,860/- lakini kwa kupendelewa au kwa wizi tu amekuwa akilipwa mshahara wa Sh.750,000/- toka Agosti 2006 alipoajiriwa.

Mwingine ambaye mshahara wake ni Sh.622,578 /-amekuwa akijilipa au kulipwa mshahara huo pamoja na mshahara mwingine wa Sh.700,000/- kila mwezi.

Mfanyakazi huyo hulipwa mishahara hiyo kwa ustadi mkubwa kwa kupitia akaunti za Chuo hicho za benki mbili tofauti.

Aidha, uchunguzi unaonesha kuwa mfanyakazi wa tatu ambaye tayari amekwisha acha kazi Muce, licha ya kuwa mshahara wake ulikuwa wa Sh.911,060/- pia alikuwa akichota mshahara mwingine wa Sh.507,590/- kupitia akaunti ya benki nyingine.

Aidha, tumeshindwa kuwataja wafanyakazi hao kwa majina kutokana na kushindwa kuwapata ili kutoa upande wao kwa kuwa mmoja yuko Tanga likizo, mwingine kaacha kazi hivi karibuni kwa notisi fupi na mwingine yuko rumande akikabiliwa na kesi nyingine.

Hata hivyo, kuhusu madai hayo ya kulipana mishahara mara mbili,Mkuu wa Chuo hicho,Professa Phillemon Mushi alikiri kuwabaini watuhumiwa hao na kueleza kuwa hatua zimekwishachukuliwa dhidi yao.

Hata hivyo, uchunguzi unaonesha kuwa watuhumiwa hao hawajachukuliwa hatua za kisheria zaidi ya kuondolewa katika idara walizokuwepo na kuhamishiwa idara tofauti.

Madai mengine yanayoukabili uongozi wa Chuo hicho ni wizi wa fedha za umma kupitia mikataba ya mzabuni aliyekuwa akitoa huduma moja Chuoni hapo.

Taarifa zinaonesha kuwa, kulingana na mkataba wake, malipo ya mzabuni huyo kwa mwezi ilikuwa ni dola za kimarekani 13,040/- lakini baadhi ya watumishi wa idara ya uhasibu na ugavi walikuwa wakishirikiana kulipa mara mbili kiasi hicho cha fedha.

Wizi huo ulikuwa unafanikishwa kwa ustadi mkubwa kwa kuandika hundi mbili zenye kiasi cha dola za kimarekani 13,040/- (19,951,200) kwa kila hundi huku zikionesha kuwa anayelipwa ni mzabuni huyo na kwamba wizi huo unadaiwa kufanyika kati ya mwaka 2006/2007 na 2008/2009.

”Lakini baada ya hundi hizo kuwa zimepita kila mahali kwa ajili ya kuidhinishwa, hundi moja ilikuwa inawekwa kwenye akaunti tofauti na wafanyakazi hao kugawana fedha hizo,” anasema mtoa taarifa wetu.

Nipashe imefanikiwa kupata namba za hundi na akaunti iliyokuwa inatumika kufanikisha wizi huo.

Hata hivyo,Professa Mushi alipoulizwa juu ya suala hilo alisema ni jambo la zamani (anataja mwaka 2009) na kwamba kwa sasa hilo siyo jambo la kujadiliwa.

”Jamani hebu mtuache nasi tufanye kazi basi hata kidogo hiyo Issue ni ya zamani mno, hata huyo (anataja jina la mzabuni) hayupo tena hapa chuoni,” alisema Professa Mushi.

”Unajua inaonekana mmeiba taarifa ya ukaguzi ambayo hata haikuwa imekamilika na ilikuwa siri, huyo mtu anayekuletea mambo hayo anatapatapa tu”, aliongeza Professa Mushi kwa ukali.

Aidha, yapo madai ya Chuo hicho kuendesha akaunti za muda maalum bila kuweka wazi faida inayotokana na akaunti hizo.

Uchunguzi unaonesha kuwa,mpaka Juni,mwaka jana, Chuo hicho kilikuwa kinaendesha akaunti zaidi ya nne za muda maalum ambazo zilikuwa na zaidi ya Sh.milioni 500.

Akaunti nne ambazo zipo kwenye benki moja yenye tawi mjini Iringa zinaonesha kuwa moja ilikuwa na kiasi cha Shilingi za kitanzania 10,090,999.55, inayofuata ilikuwa na Sh.201,247,671.23, pia ilikuwepo akaunti yenye Sh.252,853,107.40 na nyingine ilikuwa na Sh.75,195,042.70 ambapo jumla yake ni Sh.milioni 539,386,820.88.

Hata hivyo, awali alipohojiwa,Professa Mushi alisema aulizwe Makamu wa Mkuu wa Chuo hicho (Fedha na Utawala),Professa Machiwa kwa maelezo kuwa ndiye alikuwa anafahamu vyema.

Professa Machiwa alipohojiwa alidai kuwa akaunti hizo hazikuwa kwenye orodha ya akaunti za Chuo hicho na kwamba hakuwa anazifahamu wala kuwa na taarifa nazo.

”Hata nikikuonyesha taarifa yangu ya kila siku akaunti hizo hazimo labda kamwone mhasibu wa Chuo anaweza kuwa anataarifa zaidi,” alisema Professa Machiwa lakini kabla mwandishi hajaondoka akaamua vinginevyo:

”Hebu ngoja nimpigie mhasibu aende Benki naye akaangalie ili atuletee taarifa kama akaunti hizo ni za Mkwawa University, kwa hiyo njoo baadaye nitakupa taarifa”. Alisema.

Hata hivyo, mwandishi aliporejea Mchana wa Januari 28,mwaka huu, Professa Machiwa alisema watu wa benki walikuwa wamegoma kutoa taarifa za akaunti hizo mpaka waandikiwe barua.

”Nimeandika barua nimeshawapelekea hivyo naomba uje wiki ijayo, na kwa kuwa sitakuwepo, utakuta taarifa kwa Katibu Muhtasi wangu,” alisema .

Mwandishi wa blog hii alifuatilia kwa siku tatu mfululizo bila kupata majibu kwa Katibu Muhtasi wake na kuamua kumtafuta Professa Mushi kwa simu ambaye baada ya kuulizwa suala hilo alisema:

”Mbona Professa Machiwa ameshakujibu, usinisumbue,” alisema kwa kifupi na kukata simu.

Hata hivyo, baadaye alipiga simu tena kwa mwandishi na kueleza kuzifahamu akaunti hizo na kudai kuwa akaunti hizo zilikuwa za zamani na kwamba hivi sasa hazipo tena.

”Unaziona kama ni nyingi lakini akaunti ni moja tu yaani kila akaunti ya kwanza inapokuwa tayari faida inachukuliwa na kufunguliwa akaunti nyingine,” alisema.

Professa Mushi alifafanua kuwa fedha zilizokuwa zimewekwa kwenye akaunti ya muda maalum zilitoka kwa wafadhili ambao hata hivyo hakuwataja, ambazo zilikuwa kwa ajili ya ukarabati wa majengo lakini baada ya mkandarasi kusuasua,waliamua kuziweka kwenye akaunti ya muda maalum ili kuepusha kuzitumia kwa shughuli zingine.

DR.Kiiza Besigye aikosoa Serikali ya Uganda

Kiongozi wa upinzani nchini Uganda na mgombea kiti cha Urais Kanali Mstaafu Dr Kiiza Besigye ameikosoa serikali ya sasa ya National Resistance Movement –NRM, kwa kupuuza malengo yaliyosababisha vita vya msituni ambavyo hatimae vilisababisha kundi la uasi a NRM kutwaa madaraka miaka 30 iliopita.

Ameyasema katika mkutano na waandishi habari mjini Kampala, akitoa ujumbe kwa jeshi hilo wakati likijiandaa kusherehekea miaka 30 ya kuasisiwa. Sherehe hizo zitafanyika mwishoni mwa juma.

Kiiza Besigye ambae zamani alikuwa katika jeshi la taifa na sasa ni mkosoaji kuu wa serikali hiyo, ameishutumu serikali ya NRM kwa kupoteza lengo la kile walichopigania wakati walipoanzisha mapambano miaka 30 iliopita.

Besigye alikuwa anagusia siku ya tarehe sita ambayo itasherehekewa Jumapili.

Katika hali inayosemekana kama kutumiwa jeshi kumpendelea mpinzani wake wa chama tawala cha NRM, Rais Yoweri Museveni, Besigye ameonya wanajeshi kujizuia kutumiwa na watu ambao wanataka kuwakatisha tamaa wananchi wa Uganda.

Nalo Jeshi kwa upande wake limesema limefanya mengi tangu wakati huo kama vile uhuru wa kusema na mengine mengi.