McEddy Elroy

Tuesday, August 31, 2010

LAPF YACHANGIA MFUKO WA WANAFUNZI MKWAWA


Meneja Mwandamizi wa Masoko na Mawasiliano wa LAPF akikabidhi hundi ya Sh.300,000/-kwa Naibu wa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mkwawa-MUCE, anayeshughulikia Utawala,Professa John Machiwa.
Fedha hizo ni mchango wa LAPF katika kutunisha mfuko wa zawadi za wanafunzi wanaofanya vizuri katika masomo yao Chuoni hapo.

CHUO KIKUU MKWAWA WATEMBEZA BAKULI KUOMBA MSAADA

Agosti 31:CHUO Kikuu kishiriki cha Elimu cha Mkwawa cha Mkoani Iringa (MUCE),kimeyalilia mashirika na wahisani mbalimbali kuliokoa jahazi la Chuo hicho ambalo limeelezwa kuwa linazama kila kukicha.

Akizungmza na ugeni wa Mfuko wa Pensheni wa Serikali za Mitaa (LAPF),uliotembelea Chuoni hapo leo (Agosti 31) Mwanasheria Mwandamizi wa Chuo hicho,Alfred Nyamwangi amesema Chuo hicho kinakabiliwa na changamoto nyingi zinazowafanya ustawi wa Chuo hicho uwe wa kusuasua.

Ugeni huo pamoja na mambo mengine, ulifika Chuo hapo kuchangia mfuko wa zawadi kwa wanafunzi wanaofanya vyema katika masomo yao zawadi ambazo hutolewa katika mahafali ya Chuo hicho.

Moja ya Changamoto hizo alisema na kushindwa kuwa na miundombinu ya kuwalaza wanafunzi wote Chuoni hapo na hivyo kuwafanya wanafunzi wengi kuishi maeneo ya hatari.

Alisema miundombinu inayotumika ni ile iliyokuwa inatumika wakati ikiwa ni Shule ya sekondari ya Mkwawa.

Alisema mabweni waliyonayo, kwa mfano, yana uwezo wa kulaza wanafunzi 1060 ikiwa ni chini ya asilimia 60 ya wanafunzi wote. Chuo hicho kwa sasa kina zaidi ya wanafunzi 1,900.

Aidha, alisema hakuna jengo la utawala na kwamba wahadhiri wamekuwa wakitumia ofisi zilizokuwa za walimu wa sekondari.

“Kimsingi hatuna ofisi hata moja vivyo hivyo jengo la Utawala na hali hii imekuwa inatishia ustawi wa Chuo chetu,” alisema Nyamwangi.
Alisema Chuo hicho kinahitaji kumbi nne za mihadhara na kwamba moja ndiyo kwanza imeanza kujengwa kwa fedha za serikali na nyingine inaweza kuanza kujengwa mwakani kwa ufadhili wa Benki ya Dunia.

Kufuatia Changumoto hizo,Nyamwangi aliiomba LAPF kutumia mfumo wa Jengo, Tumia na Hamisha ambapo inaweza kuingia mkataba na Chuo hicho, ikapewa eneo la kujenga na baada ya miaka kadhaa majengo hayo yakamilikishwa kwa Chuo hicho.

Akizungumza mara baada ya kukabidhi hundi ya Sh.laki tatu kwa uongozi wa MUCE,Meneja Mwandamizi wa Masoko na Mawasiliano wa LAPF,Andrew Kuyeyana alisema licha ya kitoa kiasi hicho kidogo cha fedha kwenye mfuko wa kuwamotisha wanafunzi wa Chuo hicho, LAPF itaendelea kuchangia kwenye mfuko huo kila mwaka.

Aliuomba uongozi wa MUCE wakutane na uongozi wa LAPF ili kuona ni namna gani nzuri ya kusaidiana kutatua changamoto zinazokikabili Chuo hicho.

Aidha,Naibu Makamu wa Mkuu wa Chuo hicho, anayeshughulikia Utawala,Professa John Machiwa aliishukuru LAPF kwa kutambua umuhimu wa kuwamotisha wanafunzi lakini pia kuonyesha nia ya kuchangia katika kutatua changamoto za Chuo hicho.

Monday, August 30, 2010

JK ANAPOGOMBANIWA NA WAPIGA KURA!


JK akigombaniwa na wapigakura huko Sumbawanga a.k.a Mjini Tupa uchawi

CHADEMA WAJINUFAISHA NA MGOGORO WA CCM

Agosti 30: CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mkoa wa Iringa jana (Agosti 30) kimezindua rasmi kampeni zake huku kikitumia mpasuko wa CCM katika Manispaa ya Iringa kama mtaji wake mkubwa.

CCM Manispaa ya Iringa kinadaiwa kuwa na mpasuko unaodaiwa kuwepo baada ya Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) kumwengua Frederick Mwakalebela licha ya kuongoza katika kura za maoni na kumweka aliyeshika nafasi ya pili,Monica Mbega ambaye pia alikuwa Mbunge wa jimbo hilo.

Akizungumza katika mkutano wa kampeni katika viwanja vya Mwembetogwa, Manispaa ya Iringa, Mgombea wa CHADEMA,Mchugaji Peter Msigwa aliwaomba wanachama na wafuasi wa CCM kumkataa mgombea wa chama hicho,Monica Mbega kwa sababu siyo chaguo lao.

Msigwa huku akishangiliwa na maelfu ya wananchi waliohudhuria mkutano huo wa kampeni, alisema imekuwa ni kawaida kwa CCM kuwachagulia wananchi mgombea na kuwataka wananchi wa jimbo la Iringa Mjini kutodanganyika.

“Kwa niaba ya familia yangu na kwa niaba ya chama changu (CHADEMA), tunampa pole sana Mwakalebela kwa kuonewa na NEC ya CCM lakini tunawaomba wananchi wa Iringa, mfuteni machozi ndugu yetu huyu (Mwakalebela) kwa kuinyima kura CCM,” alisema Mchungaji Msigwa.

Mchungaji Msigwa ambaye uchaguzi wa mwaka 2005 aligombea jimbo hilo kupitia chama cha Tanzania Labour (TLP) alisema endapo atachaguliwa atawatumikia wananchi wa Manispaa ya Iringa kwa unyenyekevu mkubwa kwa sababu wao ndiyo waajiri wake.

Alisema atatumia vitivo mbalimbali vya Vyuo Vikuu vilivyopo Manispaa ya Iringa kuviunganisha na wananchi katika harakati ya kuvitumia Vyuo hivyo kuleta maendeleo.

Wengine waliohudhuria uzinduzi huo ni pamoja na aliyekuwa kada wa CCM ambaye ametimkia CHADEMA na anagombea Jimbo la Njombe Kaskazini,Alatanga Nyagawa.

Nyagawa alijinasibu kuwa yeye, msigwa pamoja na aliyekuwa kada mwingine wa CCM aliyetimkia Chadema,Thomas Nyimbo tayari ni wabunge kutokana na kile alichokieleza kuwa wapinzania wao ni dhaifu.

“Tutatumia udhaifu wa wagombea wenzetu kushinda kwa kishindo,” alisema.

Moja ya udhaifu wa mgombea wa CCM katika jimbo la Njombe Kaskazini ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa Iringa,Deo Sanga maarufu Jah People,ni kudaiwa kuwa na elimu ya darasa la pili.

“Nitawaomba wananchi wa Njombe Kaskazini wamnyime kura Deo Sanga ili arudi MEMKWA (mpango maalum wa elimu kwa walioikosa),” alisema.

Hata hivyo,Sanga mwenyewe alipoongea na BLOG HII kwa simu alikanusha madai kwamba elimu yake ni darasa la pili bali akasema elimu yake ni darasa la saba na kwamba alisoma katika shule ya msingi Ikwega iliyopo wilayani Mufindi, ingawa alisema hakumbuki alihitimu mwaka gani.

“Mpaka nirejee kwenye kumbukumbu zangu ndiyo naweza kukueleza nilianza mwaka gani na nikamaliza mwaka gani,” alisema Deo Sanga, hata hivyo alipotafutwa baadaye alikuwa hapatikani.

Hata hivyo, alisema Nyagawa anayedai kwamba yeye (Sanga) ni mbumbumbu ni mfa maji anayetapatapa baada ya kuangushwa katika kura za maoni za CCM na kukumbilia CHADEMA.

WAODAI STAKABADHI KUBANWA NA SHERIA

Agosti 30:MAMLAKA ya Mapato (TRA) Mkoa wa Iringa imewatahadharisha wananchi kuwa watakumbana na mkono wa sheria ikiwa wataendelea kununua bidhaa mbalimbali bila kudai sitakabadhi ya manunuzi yao.

Akizungumza na blog hii ofisini kwake,Menaja wa TRA Mkoa wa Iringa,Rosalia Mwenda alisema sheria iliyowezesha kuwepo kwa mashine maalumu za kielektroniki (EFD) za kutoa stakabadhi na kutunza kumbukumbu, inambana pia mnunuzi kudai risiti kwa kila bidhaa anayouziwa.

Kwa mujibu wa Meneja huyo, sheria hiyo inawataka wafanyabiashara wote walioandikishwa na kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kufunga mashine hizo kwenye maeneo yao ya biashara.

“Moja ya vikwazo vya kukusanya kodi ambavyo vimetukabili muda mrefu ni wananchi kutokuwa na utamaduni wa kudai syakabadhi, kwa bahati nzuri sheria ya mashine hizi za EFD inambana pia mtu ambaye atakuwa na bidhaa lakini akiwa hana stakabadhi, hivyo tunaomba wananchi kila wanaponunua bidhaa wadai stakabadhi vinginevyo watashitakiwa mahakamani” alisema.

Alisema EFD (Electronic Fiscal Device) ni mashine ambayo hutoa stakabadhi na kutunza kumbukumbu za kibiashara kwa muda wa miaka mitano na pia zitakuwa zinatoa taarifa TRA juu shughuli zote za kibiashara zinazofanywa na mfanyabiashara mwenye mashine hiyo kwa njia ya kielektroniki.

Alisema mwaka huu wa fedha yaani kuanzia Julai, 2010 hadi Juni 2011 TRA Mkoa wa Iringa imepangiwa kukusanya zaidi ya Sh.bilioni 23.112 ikiwa ni ongezeko la asilimia 32 ikilinganishwa na lengo la mwaka wa fedha wa 2009/2010.

Alisema mwaka wa fedha wa 2009/2010 walipangiwa kukusanya Sh.bilioni 16.773 lakini wakavuka lengo kwa kukusanya Sh.bilioni 17.663 sawa na asilimia 105 ya lengo.

Mwenda alisema waliweza kuvuka lengo kutokana na mikakati waliyojiwekea na kuitekeleza vyema ikiwa ni pamoja na kuweza kutekeleza shughuli ya ukaguaji wa hesabu za walipakodi hali iliyowaongezea makusanyo ya kodi.

Mkakati mwingine ni ukusanyaji kodi kwa vitalu, yaani maafisa wa TRA wamekuwa na utaratibu wa kuangalia hali halisi ya baishara za wafanyabiashara ikilinganishwa na nyuma ambapo wafanyabiashara wenyewe ndiyo walikuwa wanatamka kiwango cha mtaji walichonacho na kukadiriwa kodi.

Alisema elimu kwa mlipakodi imewasaidia pamoja na ushirikiano miongoni mwa wafanyakazi imekuwa ni chachu hiyo ya kuvuka lengo.

Sunday, August 29, 2010

MWAMUZI WEBB WA UINGEREZA ALIPOCHEMSHA SAUZI


De Jong wa timu ya Taifa ya Uholanzi akimrushia daluga Alonso wa timu ya Taifa ya Uhispania.
Mwamuzi aliyechezesha mechi hiyo ya fainali kule kwa mzee wetu Madiba, muingereza Howard Webb amekiri kuwa,De Jong alistahili kadi nyekudu badala ya njano aliyompa.
Chonde chonde waamuzi, kuwenu makini ili tufaidi burudani hii ya dunia.

Friday, August 27, 2010

TLP IRINGA WATIMULIWA KWENYE JENGO

CHAMA cha Tanzania Labour (TLP) Mkoa wa Iringa, kimepata pigo baada ya ofisi yake kufungwa na samani zote za ofisi hiyo kushikiliwa kwa ajili ya kupigwa mnada na kampuni ya udalali ya Majembe.

TLP iliyokuwa imeweka Ofisi zake katika jengo la Akiba House linalomilikiwa na Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF) hadi sasa haina Ofisi na hivyo kuwafanya viongozi wake kuhaha mitaani.

Ofisi hiyo ilivunjwa juzi na vifaa vyote kuchukuliwa na Kampuniya Majembe ikiwemo mafaili na nyaraka mbalimbali kutoka na Chama hicho kudaiwa pango la zaidi ya Shilingi 2,400,000.

Jana mchana Nipashe iliwashuhudia watumishi wa kampuni ya udalali ya majembe wakiondoa samani za ofisi hiyo na kuzipakia kwenye magari yao na kisha kuifunga ofisi hiyo kwa makufuli maalumu.

Katibu wa TLP Mkoa wa Iringa, Mrisho Samson na Katibu Mwenezi wa Mkoa huo Francis Blanka walifika baadaye ofisini hapo na kujaribu kuoko baadhi ya nyaraka lakini walikataliwa na wafanyakazi hao wa Majembe.

Meneja wa Operesheni wa Majembe, Mussa Moto hakutaka kuzungumzia suala hilo kwa madai kwamba jambo hilo waulizwe NSSF ndiyo waliowapa kazi hiyo ya kuwatoa baadhi ya wapangaji.

Kwa upande wake,Meneja wa NSSF Mkoa wa Iringa, Bathow Mmuni, alisema hawakuwa na lengo lolote la kisiasa dhidi ya TLP bali wako kwenye operesheni ya kukusanya madeni kutoka kwa wadaiwa sugu.

Alisema TLP ni mmoja wa wapangaji ambao ni wadaiwa sugu katika jengo hilo la ‘Akiba House’ na kwamba hawakuwa na njia mbadala bali ni kuwaondoa kwenye jengo kutokana na kushindwa kulipa kodi kwa zaidi ya miaka miwili.

Alisema katika operesheni hiyo,jumla ya wapangaji 33 waliopo kwenye majengo mbalimbali ya vitega uchumi vya NSSF Mkoani Iringa, walikuwa ni wadaiwa sugu ambapo baada ya shughuli hiyo ya kukusanya madeni kukabidhiwa kwa Majembe Auction Mart,zaidi ya Sh.milioni 54.5 zimekusanya.

Alisema wapamgaji tisa wakiwemo TLP ambao wameshindwa kulipa madeni, wameondolewa kwa nguvu na mali zao hususani samani za ofisi zimetaifishwa mpaka watakapolipa madeni na wakishindwa samani hizo zitauzwa kwa mnada.

Katibu wa Mkoa wa TLP,Samson hakutaka kulizungumzia suala hilo kwa maelezo kuwa siyo msemaji lakini Katibu Mwenezi,Blanka alikiri TLP kudaiwa Sh.2,400,000 ikiwa ni kodi ya pango.

Hata hivyo, alisema Chama chake (TLP) Taifa kimeshakiri kulitambua deni hilo na walikuwa wameandika barua kwa NSSF kwamba watachelewa kidogo kulipa kwa sababu Mwenyekiti wa Taifa,Agustino Mrema ambaye alipaswa kusaini hundi ya malipo hayupo Dar-es-Salaam.

Mrema Mwenyewe alipopigiwa Simu alijibu kwa kifupi tu kisha kukata simu: “Mimi nahangaikia Jimbo langu la Vunjo bwana hayo mambo ya ofisi siyajuwi”.

TLP ni moja ya vyama vya upinzani vilivyosimamisha wagombea wa ubunge katika Jimbo la Kalenga na katika majimbo mengine kimekuwa pega kwa pega kuwaunga mkono wagombea wengine wa vyama vya upizani na sasa kimetaifishwa ofisi ya kuratibu shughuli hizo za kampeni.

Tuesday, August 24, 2010

HILI SIYO BANDA LA KUKU NI BWENI!

Wanafunzi wapatao 100 wa shule ya sekondari ya Bomalang'ombe wilayani Kilolo inayomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri nchini (KKKT) Dayosisi ya Iringa walikuwa wakilitumia 'kujisomea' usiku na wakilala humu kabla waumini wa kanisa hilo wa nchini marekani hawajatoa fedha kwa ya ujenzi wa bweni zuri. Jiulize Mwenyewe,mwanafunzi anayejisomea kwenye bweni hili na kulala humo, atafaulu mtihani wake wa kidato cha nne?.

Tafakari,Chukua hatua!

Wageni waliofika kujionea Bweni lililojengwa kwa kutumia mabaki ya magogo ya mbao maarufu 'mabanzi' wengi wao kutoka Marekani.
Wageni hawa pamoja na mambo mengine,walifika kujionea bweni hilo pia kushuhudia uzinduzi wa bweni la heshima la utu lililojengwa kwa ufadhili wa fedha zao ili kuwaokoa wanafunzi waliokuwa wakilala kwenye bweni hilo la mateso makubwa.

Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya Bomalang'ombe wilayani Kilolo wakisherehekea uzinduzi wa bweni jipya lililojengwa karibu kabisa na bweni la mabanzi walilokuwa wanatumia awali.
Bweni hili jipya lilipewa jina la 'Bweni la Miujiza' kutokana na kujengwa harakaharaka tena wakati wa mvua ili kuwaokoa wanafunzi hawa waliokuwa wanaumia kwa baridi kali hususani wakati wa usiku.

Thursday, August 19, 2010

NIPENI TENA WANYALUKOLO 'BAYANGU'

Aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Kilolo,Prof.Peter Msolla (Kulia) akirejesha fomu za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuomba kuwania tena jimbo hilo kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi. Anayepokea fomu hizo ni Msimamizi wa uchanguzi jimbo la Kilolo ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa wilaya hiyo,Bosco Nduguru.

KIPYENGA CHAPULIZWA RASMI MAJIMBONI

Agosti 19:VIGOGO wawili wa CCM wa Mkoani Iringa waliotimkia Chadema,Alatanga Nyagawa na Thomas Nyimbo wamerejesha fomu za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) za kuwania ubunge kwa tikiti ya chama hicho katika Majimbo ya Njombe Kaskazini na Njombe Magharibi.

Tofauti na Majimbo mengine, kama watapitishwa na NEC, watakaopambana Jimbo la Njombe kaskazini ni Deo Sanga, ambaye ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa na Alatanga Nyagawa wa Chadema.

Aidha,Jimbo la Njombe Magharibi watakaopambana pia ni wawili tu ambao ni Thomas Nyimbo wa Chadema ambaye amewahi kuwa Mbunge wa Jimbo hilo kwa tikiti ya CCM kwa kipindi cha miaka kumi ambaye atapambana Gelson Lwengwe wa CCM.

Kwa upande wa kilolo, Prof.Peter Msolla ambaye wakati akirejesha fomu mamia ya watu waliandama naye, atapambana na Cray Mwituka wa Chadema na mwana mama Mwaka Mgimwa wa chama cha Chausta.

“Nawashukuru wananchi kwa kuonesha imani kwangu na nitajihadi kuwahudumia vyema ili niwe mbunge wao wa kudumu kama wanavyoomba,” alisema Msolla ambaye alikuwa akijibu maombi ya wananchi waliokuwa wakiimba kutaka awe mbunge wao wa kudumu.

Wengine waliorejesha fomu hadi jana saa 9:00 alasiri ni kama ifuatavyo:

Mufindi Kusini.
Menrad Kingola (CCM).

Mufindi Kasikazini.
Mahamud Mgimwa (CCM) na Lawrance Mwabusi (NCCR-Mageuzi).

Jimbo la Kalenga.
Dr.William Mgimwa (CCM),Rehema Makoga (Chadema), Makuke Mginja (Jahazi Asilia) na John Lumuliko (TLP).

Jimbo la Isimani.
Benny Kapwani (Chadema), William Lukuvi (CCM) na Mussa Fufumbe (CUF).

Jimbo la Iringa Mjini.
Monica Mbega (CCM) na Mchungaji Peter Msigwa (Chadema).

Mwisho.

Wednesday, August 18, 2010

UNAWAKUMBUKA HAWA?

Kuanzia kushoto, Marehemu Mwalimu Julius Nyerere, Mzee John Malecela,Njelu Kasaka na Marehemu Peter Siyovelwa.

Tuesday, August 17, 2010

Mwakalebela na Mkewe wakiwa mahakamani


Mwakalebela kwa pamoja na mkewe wakiwa kizimbani katika mahakama ya Mkoa wa Iringa kujibu tuhuma zinazowakabili

MASHITAKA DHIDI YA MWAKALEBELA

HATIMAYE Kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Frederick Mwakalebela (41) na mkewe Selina Mwakalebela, wanaokabiliwa na tuhuma ya rushwa katika mchakato wa kura za maoni za kumpata mgombea ubunge wa chama hicho Jimbo la Iringa Mjini, wamefikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.
Awali,Mwakalebela alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilayani Iringa, kwa ajili ya kusomewa shitaka la kwanza ambalo ni kesi ya Jinai namba 4 ya mwaka 2010, inayohusiana na kutoa hongo kinyume cha sheria namba 15 (1) (b) ya sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ambayo ilisomwa pamoja na kifungu cha cha 21 (1) ( a) na 24 (8) ya Sheria ya gharama za Uchaguzi.
Kesi hiyo ilikuwa ikisikilizwa na Hakimu Festo Lwila wa Mahakama ya Hakimu mkazi Wilaya ya Iringa.
Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Imani Nitume aliyekuwa akisaidiwa na Prisca Mpeka alidai kuwa Mwakalebela alitenda kosa hilo mwezi Juni mwaka huu katika kijiji cha Mkoga katika Manispaa ya Iringa.

Mwakalebela anadaiwa kutoa hongo ya Sh.100,000 kwa Mwenyekiti wa kijiji hicho, Hamisi Luhanga ili azigawe kwa wapiga kura 30 wa CCM ili wampigie kura za maoni za kumchagua mtuhumiwa wa kwanza (Mwakalebela), 01/08/2010 .

Mtuhumiwa huyo alikana kosa hilo na Hakimu Lwila alisema dhamana iko wazi kwa Mwakalebela ambapo alitoa masharti ya dhamana hiyo ambayo ni pamoja na ahadi ya shilingi milioni 5000,000 kwa kila mdhamini.

Mwakalebela alidhaminiwa na wadhamini wawili ambao mmoja wao ni mtumishi wa Serikali. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Septemba 15 mwaka huu itakapotajwa tena.

Katika kesi ya pili namba 8, ya mwaka 2010,inayomkabili pia mtuhumiwa Frederick Mwakalebela na Mkewe Selina Mwakalebela, Mwendesha Mashitaka wa Takukuru Imani Nitume alidai mbele ya mahakama hiyo kuwa watuhumiwa hao kwa pamoja wanakabiliwa na kosa la kutoa hongo ya shilingi 100,000 kinyume na vifungu vilivyotajwa hapo juu.

Kesi hiyo inasikilizwa na Hakimu mkazi Mkoa wa Iringa, Gladys Barthy.

Hata hivyo,wakati kesi hiyo ikiendelea, yalijitokeza mabishano ya kisheria kati ya Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Imani Nitume na Wakili wa Kujitegemea Basil Mkwata anayemtetea Mwakalebela na mkewe Selina, kutokana na mahakama kutaka kujiridhisha na nyaraka zilizotumiwa na baadhi ya wadhamini.

Baadhi ya nyaraka za wadhamini (barua) waliojitokeza mahakamani hapo zilikuwa hazijakamilika na Mwendesha mashitaka wa Takukuru na Wakili huyo walikuwa wakibishana kuhusiana na utata huo, ingawa baadae walipatatikana wadhamini waliokuwa na nyaraka timilifu.

Watuhumiwa wote wawili wamekana kosa hilo na wameachiwa kwa dhamana hadi hapo kesi hiyo itakapotajwa tena Septemba 15 mwaka huu.

MWAKALEMBELA AKISUBIRI KUPANDA KIZIMBANI


Frederick Mwakalebela akisubiri kupandishwa kizimbani, nyuma ni wapambe na wafuasi wake wa Mjini Iringa wakiwa wanasubiri kwa hamu kusikia mashitaka yanayomkabili Swaiba wao.

Mwakalebela atinga Mahakamani



Aliyekuwa mgombea wa ubunge katika jimbo la Iringa Mjini kwa tikiti ya CCM,Frederick Mwakalebela, mkewe Selina Mwakalebela na wapambe wake wakiwasili katika 'Uwanja wa Haki' wa Mkoa wa Iringa a.k.a Mahakama ya Mkoa wa Iringa kujibu mashitaka yanayomkabili ya kutoa hongo katika mchakato wa kura za maoni.

Sunday, August 15, 2010

MCHUNGAJI MKWARE AFUTWA KAZI NA DAYOSISI

Na Mawazo Malembeka,Iringa

Agosti 15:KANISA la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Iringa, limemfuta kazi mwalimu na Mchungaji Michael Ngilangwa (35) anayekabiliwa na kesi mahakamani ya kuomba rushwa ya ngono na kutaka kumbaka mwanafunzi mwenye umri wa miaka 14 wa kidato cha kwanza wa shule ya sekondari ya Pomerin inayomilikiwa na Kanisa hilo.

Ngilagwa ambaye ni mwalimu wa kingiireza na masomo ya dini katika shule hiyo, alikamatwa Agosti 11, mwaka huu na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Iringa akiwa nyumba ya kulala wageni iitwayo Wihanzi akiwa na mwanafunzi huyo.

Agosti 13, mwaka huu, Ngalingwa, alipandishwa kizimbani katika mahakama ya Mkoa wa Iringa na kusomewa mashitaka mawili ya kuomba rushwa ya ngono kwa binti mwenye umri wa miaka 14 kinyume cha sheria ya Kuzuia na kupambana na rushwa ya mwaka 2007 na kutaka kubaka kinyume na sheria ya jinai namba 16 ya mwaka 2002.

Akizungumza na Nipashe, Katibu Mkuu wa Dayosisi ya Iringa (DIRA), Nayman Chavalla alisema ofisi yake imemfuta kazi mwalimu huyo tangu Agosti 13,mwaka huu.

Alisema wamemfuta kazi kutokana na kufanya kitendo ambacho hakiungwi mkono na Kanisa, Dayosisi na wala shule ya Sekondari ya Pomerin.

“Kile kitendo tu cha kukutwa na mwanafunzi wake nyumba ya kulala wageni, tena usiku, kinatosha kutufanya sisi (DIRA) tuchukue maamuzi ambayo tumeona yanafaa, nayo ni kumfuta kazi mara moja,” alisema Chavalla.

Hata hivyo Chavalla alisema kuwa Ngilangwa hakuajiliwa kama Mchungaji na kwamba kwenye orodha ya wachungajiwa wa DIRA hayumo bali yumo kwenye orodha ya walimu wa DIRA.

Alisema mwalimu huyo ana shahada ya dini (Theolojia) na ni mwanafunzi wa shahada ya ualimu katika Chuo Kikuu huria na kwamba pale Pomerin aliajiliwa kama mwalimu.

Aidha, alisema kuwa, suala la Ngilangwa kufanya kitendo hicho kichafu, ni jambo binafsi na kwamba halina uhusiano wa shule, Dayosisi wala Kanisa.

“Utaona tangu suala hili likiwa mikononi mwa Takukuru hadi mahakamani, hakuna mtumishi wa shule, Dayosisi wala Kanisa aliyekwenda huko kutoa msaada wa aina yoyote,” alisema Chavalla.

Mwisho.

Friday, August 13, 2010

MHASIBU WAKALA WA MAJENZI CORKOTINI

Na Mawazo Malembeka,Iringa

Agosti 13: MHASIBU Msaidizi wa Wakala wa Majenzi (TBA) Mkoa wa Iringa,Benjamin Mbope (56),amepandishwa kizimbani kwa makosa 94 ya kula njama, kughushi na kuibia wakala hao zaidi ya Sh.35.3

Mhasibu huyo msaidizi amefikishwa mahakamani jana (Agosti 12) katika mahakama ya wilaya ya Iringa.

Mbele ya Hakimu wa mahakama hiyo,Festo Lwila,Mwendesha mashitaka,Mrakibu msaidizi wa polisi,Matiku, alidai kuwa, kati ya Disemba 2, mwaka jana na Juni 8,mwaka huu, mtuhumiwa alitenda makosa hayo.

Matiku alidai kuwa, Desemba 2 mwaka jana, kwa nia ya kuidhulumu wakala hiyo, mtuhumiwa alikula njama na watu wasiojulikana na kuiba jumla ya Sh.35,377,300.

Aidha, Matiku aliendelea kuieleza mahakama hiyo kwamba, Desemba 23, mwaka jana, mtuhumiwa alighushi saini ya Meneja wa Wakala hiyo, Bartazar Kimangano na kuiba Sh.1,780,300 huku akijua kuwa ni kosa la jinai.

Mahakama hiyo iliendelea kuelezwa kwamba, Mhasibu huyo msaidizi aliandaa na hatimaye kuandika cheki yenye namba 3896729 na kuiba kiasi hicho cha fedha kutoka kwenye akaunti ya wakala hiyo yenye namba 01J1027842011 iliyopo benki ya CRDB Mkoa wa Iringa.

Katika kosa la kumi hadi 94, ilielezwa mahakamani hapo kwamba kati ya Disemba mwaka jana na Juni mwaka huu, mtuhumiwa huyo kwa nyakati tofauti alikuwa akiandaa hati za malipo na kuandika cheki na kuiba viwango tofauti tofauti cha fedha kinachofikia zaidi ya Sh.milioni 35.3.

Upande wa mashitaka ulisema dhamana kwa mtuhumiwa iko wazi ikiwa mtuhumiwa angetimiza masharti yatakayowekwa na mahakama.

Akisoma masharti ya dhamana, hakimu Lwila alisema mtuhumiwa alitakiwa kuwa na wadhamini wawili ambao kila mmoja amdhamini mtuhumiwa kwa Sh.milioni 40 na kwamba mmoja wa wadhamini hao lazima awe na mali isiyohamishika katika Manispaa ya Iringa, yenye thamani ya Sh.milioni 30.

Mtuhumiwa alishindwa kutimiza masharti ya dhamana na alipelekwa gereza la mahabusu hadi Agosti 26,shauri hilo litakapolejeshwa mahakamani hapo kwa kutajwa.

Mwisho.

Thursday, August 12, 2010

MAKADA WA CCM ZAIDI CORTIN, MWALIMU ANASWA KWA RUSHWA YA NGONO

Na Mawazo Malembeka

Agosti 12:MTUHUMIWA mwingine wa rushwa katika kura za maoni katika jimbo la Iringa Mjini,ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Mkoa wa Iringa,Fadhili Ngajilo, leo amepandishwa kizimbani kujibu tuhuma zinazomkabili.

Ngajilo (31), ambaye pia ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu John cha Mjini Dodoma, alifikishwa mahakama ya Mkoa wa Iringa na kusomewa shitaka moja la kutoa hongo kinyume na sheria namba 11 ya kupambana na kuzuia rushwa ya mwaka 2007 na sheria ya gharama za uchaguzi ya mwaka 2010.

Mbele ya hakimu wa mahakama hiyo, Consolatha Singano, Mwanasheria wa Takukuru,Prisca Mpepo alidai kuwa Ngajilo anadai kutoa hongo hiyo Julai 20,mwaka huu katika kijiji cha Mgongo,Manispaa ya Iringa.

Mwanasheria huyo alidai kuwa Ngajilo anadaiwa kutoa hongo ya Sh.30,000 kwa Kaimu Katibu wa CCM tawi la Mgogo,Gwido Sanga ili naye azigawe kwa wajumbe 30 wa CCM waliokuwa wamekusanyika kwenye nyumba ya Damas Mbilinyi kusubiri wagombea waliokuwa wanapita eneo hilo kujinadi.

Alidai kuwa hongo hiyo ililenga kuwashawishi wajumbe hao wampigie kura Ngajilo wakati wa kupiga kura za maoni.

Mtuhumiwa huyo alikana shtaka dhidi yake na Mwanasheria wa Takukuru, Prisca, alidai mahakamani hapo kwamba upelelezi haujakamilika na kwamba dhamana iko wazi kwa mtuhumiwa kama angetimiza masharti ambayo yangewekwa na mahakama hiyo.

Akisoma masharti ya dhamana kwa mtuhumiwa, hakimu Singano alisema mtuhumiwa alitakiwa kuwa na wadhamini wawili ambao ni wakazi wa Mkoa wa Iringa ambao pia wawe watumishi wa Serikali au taasisi yoyote inayotambulika kisheria na kwamba kila mdhamini asaini dhamana ya Sh.milioni mbili.

Hata hivyo, Ngajilo aliyekuwa anaonekana kujiamini muda wote wakati shaurio lake likisomwa, alikuwa ameandaa wadhamini wawili lakini mmoja ambaye alidaiwa kuwa ni baba yake alikataliwa na mahakama hiyo kwa kuwa nyaraka zake zilithibitisha kwamba siyo mtumishi wa serikali.

Hakimu Singano aliahirisha shauri hilo hadi Septemba 06,mwaka huu, litakapotajwa tena na Ngajilo aliwekwa mahabusu wakati akisubiri kukamilisha taratibu za dhamana ambapo hadi majira saa saba mchana, alikuwa bado hajakamilisha taratibu hizo.

Watuhumiwa wengine kufikishwa mahakamani jana ni pamoja aliyewahi kuwa waziri kwa nyakati tofautitofauti na Mbunge wa siku nyingi wa jimbo la Mufindi Kaskazini,Joseph Munga akikabiliwa na makosa 15 ya rushwa.

Mwingine ni Frederick Mwakalebela ambaye licha ya kutokuwepo mahakama kwa taarifa, kesi yake ilifikishwa mahakamani na kusogezwa mbele hadi Agosti17,mwaka huu.

Wakati huo huo, Takukuru inamshikilia Mwalimu wa shule ya sekondari ya Pomerin iliyoko wilayani Kilolo inayomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Iringa,Michael Ngalingwa (35) kwa tuhuma ya kuomba na kupewa rushwa ya ngono kutoka kwa mwanafunzi wake wa kidato cha kwanza.

Taarifa zilizothibitishwa na Kaimu Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Iringa,Gasto Mkono, mwalimu huyo anadaiwa kuomba rushwa ya ngono kwa mwanafunzi wa kidato cha kwanza ili amsadie kufaulu vyema somo la kiingereza pamoja na kumpa ahadi ya kumsaidia matumizi madogomadogo awapo shuleni hapo.

Kwa mujibu wa Mkono, Takukuru walipewa taarifa za tukio hilo na wasamalia wema na kuweka mtego ulifanikiwa kumnasa mwalimu huyo kwenye moja ya nyumba za kulala wageni Mjini Iringa, saa sita ya usiku wa kuamkia leo (Agosti 12) akiwa na binti huyo.

Mkuu wa shule hiyo ya Pomerin, Shadrack Nyaulingo hakupatikana kwa maelezo kuwa alikuwa njia kwenda Takukuru kutoa baadhi ya taarifa muhimu zinazohusiana na tukio hilo.

Hata hivyo,msemaji mmoja wa Ofisi ya Dayosisi ya Iringa, (DIRA), ambaye hakupenda jina lake litajwe kwa maelezo kuwa ofisi hiyo haihusiki na sula hilo kwa kuwa ni la binafsi zaidi (la Mwalimu aliyekamatwa) alikiri kuwepo kwa tukio hilo.

“Hata sisi tumepata taarifa hizi, ni kweli lakini naomba mtafute Mkuu wa shule atakueleza vyema, sisi (DIRA) hatuhusiki nalo kwa sababu ni la binafsi sana,” alisema kwa upole.

Mwisho

Wednesday, August 11, 2010

TAKUKURU IRINGA YAANZA KAZI,MUNGAI CORTINI

Agosti 11:TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) leo imeanza rasmi kuwapandisha kizimbani makada wa CCM waliotuhumiwa kutoa rushwa wakati wa kampeni za kura za maoni kuomba kuteuliwa kukiwakilisha Chama hicho katika nafasi ya ubunge kwenye majimbo yao.

Waliokuwa wa mwanzo kuonja shubiri hiyo ya kupandishwa kizimbani ni pamoja na Mbunge wa Mufindi Kaskazini,Joseph Mungai na aliyeongoza kura za maoni jimbo la Iringa mjini,Frederick Mwakalebela.

Mungai (66), kwa pamoja na watu wengine wawili ambao ni pamoja na Katibu wa Umoja wa vijana wa CCM wa wilaya ya Mufindi,Fidel Cholela (39) na Moses Masasi wamefikishwa katika mahakama ya Mkoa wa Iringa wakikabiliwa na mashtaka 15 ya rushwa kinyume na sheria ya kuzuia na kupamna na rushwa ya mwaka 2007 na sheria ya gharama za uchaguzi ya mwaka 2010 .

Kwa upande wa Mwakalebela, shauri lake lenye tuhuma moja ya rushwa, limefikishwa katika mahakama hiyo ya Mkoa lakini limesongezwa mbele hadi Adosti 17,mwaka huu, kwa kuwa alikuwa na ruksa ya kutokuwepo mahakamani leo.

Mbele ya hakimu wa mahakama ya Mkoa wa Iringa,Merry Senapee, msoma mashtaka wa Takukuru,Prisca Mpepo alidai kuwa mnamo Julai 08,mwaka huu, katika kata ya Ihalimba, wilaya ya Mufindi, Mungai akiwa mmoja wa makada wa CCM waliokuwa wanawania kupitishwa katika kura za maoni kugombe ubunge wa jimbo la Mufindi Kaskazini kwa pamoja na watuhumiwa wenzake, walitoa hongo ya Sh.10,000 kwa Mwenyekiti wa CCM tawi la Vikula kama kishawishi cha kumpigia kura wakati wa zoezi la kura za maoni.

Katika shtaka la pili, watuhumiwa wote kwa pamoja, siku na eneo hilo walitoa hongo ya Sh.10,000 kwa Konjesta Kiyeyeu ambaye alihudhuria kikao cha kamati ya CCM kijiji cha Vikula.

Msoma mashtaka aliendelea kudaia mahakamani hapo kuwa, katika shtaka la tatu, nne, tano na sita, watuhumiwa wanadaiwa kutoa hongo ya Sh.10,000/- kwa kila mmoja kwa Aldo Lugusi, Ezekiel Mhewa, Tulaigwa Kisinda na Jiston Mhagama kwa lengo hilihilo la kuwashawishi wampigie kura za maoni.

Shtaka la saba wanadaiwa kutoa hongo ya Sh.20,000 kwa Maria Kihongosi na shtaka la nane kutoa hongo ya Sh.5,000 Lurent Mdalingwa wakati shtaka la tisa wanadaiwa kutoa hongo ya Sh.20,000 kwa Victory Kalinga ambaye ni Mwenyekiti wa CCM kijiji cha Ugessa.

Katika mashtaka namba kumi hadi 12 washtakiwa wote kwa pamoja wanadaiwa walitoa hongo ya Sh.2,000 kwa kila mmoja kwa Francis Chonya, Alfred Kisinga na Issac Tewele wakati shtaka la 13 wanadaiwa walitoa hongo ya Sh.10,000 kwa Sosten Kigahe.

Aidha, msoma mashtaka huyo alidai kuwa shitakana namba 14 watuhumiwa wanadaiwa kutoa hongo ya Sh.10,000 kwa Raphael Lutumo na shitaka la mwisho walitoa hongo ya Sh.20,000 kwa Andrew Mkiwa.

Watuhumiwa wote walikana mashtaka na hakimu Senapee alisema dhamana iko wazi kwa watuhumiwa kwa masharti kwamba kila mtuhumiwa awe na wadhamini wawili ambapo mmoja wa wadhamini hao awe anaishi Manispaa ya Iringa na kila mdhamini asaini bondi ya Sh.milioni tano.

Hadi wandishi wa habari hii wanatoka mahakamani majira ya saa tano asubuhi, si Mungai wala watuhumiwa wengine waliokuwa wametimiza masharti ya dhamana hivyo waliswekwa mahabusu ya mahakama wakisubiri jamaa zao kutimiza masharti ya dhamana.

Taarifa zilizopatikana baadaye majira ya saa 8.30 alasiri kutoka mahakamani hapo zilithibitisha kuwa watuhumiwa wote walitimiza masharti ya dhamana na kwamba shauri hilo litarejeshwa mahakamani hapo kwa kutajwa Agosti 25,mwaka huu.

Kwa upande wa shitaka lililofikishwa mahakamani hapo likimkabili Mwakalebela, lilidai kuwa mtuhumiwa huyo alitenda kosa la rushwa Juni, mwaka huu, katika kijiji cha Mkoga,Manispaa ya Iringa.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka ya Takukuru,Mwakalebela anadaiwa kutoa hongo ya Sh.100,000 kwa Mwenyekiti wa CCM wa kijiji hicho,Hamisi Luhanga ili naye azigawe kwa wapiga kura wa CCM ambao wangempigia kura wakati wa zoezi la kura za maoni.

Mwakalebela alikuwa na udhuru hivyo shauri lake lilisongezwa mbele hadi Agosti 17,mwaka huu.

Hata hivyo, Kamanda wa Takukuru wa Mkoa wa Iringa,Bonasian Kessy alisema Mwakalebela anashitakiwa kwa makosa mawili ya rushwa na kwamba shtaka lingine litafikishwa mahakamani kesho (Agosti 12) ingawa hakutaka kulifafanua.

Kamanda Kessy pia alithibitisha kuwa mtuhumiwa mwingine wa rushwa katika kampeni za kura za maoni ambaye ni Mwenyekiti wa Umoja wa vijana wa CCM Mkoa wa Iringa,Fadhili Ngajilo pia atapandishwa kizimbani kesho (Agosti 12) kusomewa mashtaka yanayomkabili.

Mwisho.